Skip to main content

Yana wenyewe

Makonde ya usuhuba, hayo yanao wenyewe
Yanataka waloshiba, wakapandwa na viwewe
Aimi wa nguvuhaba! sezi viwavu n'waniwe
Huba ni la wa manguvu, n'lokifyefye najitowa

N'lokifyefye najitowa, niachiye wenye nguvu
Sitwai ningapawa, nachia yangu makovu
Kumbe hayanayo dawa, yenye  kuleta utuvu
Vikumbo vyayo mapenzi, vyahitaji wenye navyo

Vyahitaji wenye navyo, wanotumia ja vyambo,
Ukicheza nao ovyo, hutohimili makumbo
Walai mja mimi sivyo, lau n'katowa matumbo
Masumbwi ya huba n'yao, wenye mbinu za mikono

Wenye mbinu za mikono, wajitenda pasi indha
Wajuzi wa mavongono, hini kwao ndio ladha
Kwazo kucha na vijino, wamewaatua kadha
Mafundo yayo mahaba, ni ya wale wasimoyo

Ni ya wale wasimoyo, walotasa wa hisia
Ndio walo na  uchoyo, waja wanojitakia
Huwezi ngapiga mbio, au kilema takutia
Una kani chache flani, kana uwachie wao

Kana uwachie wao, nakwamba ni wachokozi
Kila kito ni cha kwao, sivyo wakulize chozi
Nawajua watu zao, mbwene na yangu maozi
Bahari’no ya  mapenzi, ina papa wavumao

Ina papa wavumao, havipezi vikambare
Nashusha yangu matao, nepuke zao ndarire
Wanayo satua yao, ninawacha wasowere
Mikwato ya suhubani, ina hao masogora

Ina hao masogora, wasojuwa na hisani,
Ndio waja wenye chira, kupoka kwao ndo shani
Hawachi k’leta khasara, kuwatenga wendani
Hila zilo mapenzini, Walai zina wenyewe


Wamalwa K.W
Mlokole Mlumbi
Kamukuywa






Comments

Popular posts from this blog

Bin-Adamu

Mimi Natakadamu ino nudhumu Nikayaambe yalomuhimu Yanotaja ghilba za bin-Adamu Wa kuhalalisha yalokharamu kufaidi yake tamaa na hamumu Yalo mema kayatiya sumu Na kuwaseta walomaamumu Wakijigeuza sanamu Wakisahau wali wanadamu Kataka ibada kwa kaumu Wadhani Takwepa luhdi wakisha humu Watakinza ya Mungu Kalamu Kwamba Muhuluku hafahamu ati hiyeyuki fuadi ngumu Ila Wendelepi siku ya hukumu? Watapokwima mbele ya Hakimu Kulipiya wao udhalimu Kama si nyoto za Jehanamu? Zitakao waunguza kwa zamu Zikisha lamba mifupa na damu Watauma zanda na kujilaumu kwa wao utimamu wa wazimu ©Wamalwa

Ukila

Ukila kile kichakwe, cha mwenzio usile Ukila wa pupa ‘siwe, pupa nayo ni ndwele Ukila haramu s’tukue, cha mwendo sikitwale Ukila nla halali ‘we, cha chira na usile Usile waja kuamba, ‘kawa kauli nawe Usile ukajigamba, kukila kisichakwe Usile na kwa mafamba, litoe jasho lakwe Usile wala kuramba, na cha hila kisiliwe Kisiliwe cha litima, wasio na uwezo Kisiliwe cha yatima, chao wastahilizo Kisiliwe hata kama, wewe una uwezo Kisiliwe na cha umma, tatapika ulazo Ulazo na kwa ghiliba, huwa sumu mwenzangu, Ulazo na ukashiba, utalipa kwa Mungu Ulazo ziwezo baba, fedha za mwendo chungu Ulazo hata zi’haba, ziwe zako ndu’yangu

Siku ya Ulifi

Toka Hegi yasikika, imelia parapanda Wafike walotajika, wasilimatie kwenda Majina waliandika, na ila walizotenda Waache kuhemeka, ili siku ya ulifi Nawaasa wahusika, waziache propaganda Hifai kulalamika, kila wanakokuenda Wengine tope kupaka, jukwaani wakipanda Wakuache kupayuka, ili siku ya ulifi Wenyewe waliyataka, mbegu mbaya walipanda Na chuki waliipika, ikaiva na kuvunda Na Umma ukagawika, maovu ukajitenda Sasa wana jakajaka, ili siku ya ulifi Mahuluki bila shaka, huvuna ‘lichopanda Na maji ukiyateka, uyanywe yote mafunda Na koo ikikabika, shauriyo ‘liyaenda Ela watawajibika, ili siku ya ulifi Wacheni kutikatika, kotekote mukiranda Mwakutaka kusifika, wafuasi mwawawinda Mwashinda kunung’unika, na mambo munayapinda Ishara ya kutishika, ili siku ya Ulifi Kama ni kutakasika, ni heri mkatuenenda Ghofira mkatutaka, tukawapa tukipenda Mumwombe Mahuluka, faraja akawatenda Badala ya kutimuka, ili siku ya ulifi Hitaaihirishika, siku ya ndege kupanda Mkayajibu mashtaka, ya zenu ila...