Skip to main content

Yana wenyewe

Makonde ya usuhuba, hayo yanao wenyewe
Yanataka waloshiba, wakapandwa na viwewe
Aimi wa nguvuhaba! sezi viwavu n'waniwe
Huba ni la wa manguvu, n'lokifyefye najitowa

N'lokifyefye najitowa, niachiye wenye nguvu
Sitwai ningapawa, nachia yangu makovu
Kumbe hayanayo dawa, yenye  kuleta utuvu
Vikumbo vyayo mapenzi, vyahitaji wenye navyo

Vyahitaji wenye navyo, wanotumia ja vyambo,
Ukicheza nao ovyo, hutohimili makumbo
Walai mja mimi sivyo, lau n'katowa matumbo
Masumbwi ya huba n'yao, wenye mbinu za mikono

Wenye mbinu za mikono, wajitenda pasi indha
Wajuzi wa mavongono, hini kwao ndio ladha
Kwazo kucha na vijino, wamewaatua kadha
Mafundo yayo mahaba, ni ya wale wasimoyo

Ni ya wale wasimoyo, walotasa wa hisia
Ndio walo na  uchoyo, waja wanojitakia
Huwezi ngapiga mbio, au kilema takutia
Una kani chache flani, kana uwachie wao

Kana uwachie wao, nakwamba ni wachokozi
Kila kito ni cha kwao, sivyo wakulize chozi
Nawajua watu zao, mbwene na yangu maozi
Bahari’no ya  mapenzi, ina papa wavumao

Ina papa wavumao, havipezi vikambare
Nashusha yangu matao, nepuke zao ndarire
Wanayo satua yao, ninawacha wasowere
Mikwato ya suhubani, ina hao masogora

Ina hao masogora, wasojuwa na hisani,
Ndio waja wenye chira, kupoka kwao ndo shani
Hawachi k’leta khasara, kuwatenga wendani
Hila zilo mapenzini, Walai zina wenyewe


Wamalwa K.W
Mlokole Mlumbi
Kamukuywa






Comments

Popular posts from this blog

Bin-Adamu

Mimi Natakadamu ino nudhumu Nikayaambe yalomuhimu Yanotaja ghilba za bin-Adamu Wa kuhalalisha yalokharamu kufaidi yake tamaa na hamumu Yalo mema kayatiya sumu Na kuwaseta walomaamumu Wakijigeuza sanamu Wakisahau wali wanadamu Kataka ibada kwa kaumu Wadhani Takwepa luhdi wakisha humu Watakinza ya Mungu Kalamu Kwamba Muhuluku hafahamu ati hiyeyuki fuadi ngumu Ila Wendelepi siku ya hukumu? Watapokwima mbele ya Hakimu Kulipiya wao udhalimu Kama si nyoto za Jehanamu? Zitakao waunguza kwa zamu Zikisha lamba mifupa na damu Watauma zanda na kujilaumu kwa wao utimamu wa wazimu ©Wamalwa

Kukrani!

Shukrani! Shukrani zangu jazila, kwa chama cha NCOLTCL (nikotiko) Akawajazi jaala, kwa kutupa mualiko Tumeteremea kulla, tulosoma toka kwako Sasa tumeshalimuka, na mbinu za kufundisha Sikomi kuwahongera, walimu walofundisha walivyojifunga nira, ya maarifa kutupasha Tuzijenge mbinu bora, Kiswahili kufundisha Sasa tumeshalimuka, na mbinu za kufundisha Mambo hayo ni muhimu, mlotupasha uchao Mliyeshusha magumu, ya nadharia zao Tuboreke walimu, kwa wale tufudnishao Sasa tumeshalimuka, na mbinu za kufundisha Hongera mwalimu Kiarie, kwa kuonyesha mifano Lisanza nikusifie, kwazo sifa nono nono Alwiya zikufikie, ulivyokuwa mfano Sasa tumeshalimuka, na mbinu za kufundisha Sikusahau Atonia, kwa wako ukakamavu, Jinsi ulokakania, pasi kuonya ochovu Uneemee dunia, kwa kutupa wangavu Sasa tumeshalimuka, na mbinu za kufundisha Wanafunzi mlofika, shukrani nyingi sana Kwenu kuwa washirika, na mwiya wenu kupana Na sisi tukazoeka, na vipindi vil...

Siku ya Ulifi

Toka Hegi yasikika, imelia parapanda Wafike walotajika, wasilimatie kwenda Majina waliandika, na ila walizotenda Waache kuhemeka, ili siku ya ulifi Nawaasa wahusika, waziache propaganda Hifai kulalamika, kila wanakokuenda Wengine tope kupaka, jukwaani wakipanda Wakuache kupayuka, ili siku ya ulifi Wenyewe waliyataka, mbegu mbaya walipanda Na chuki waliipika, ikaiva na kuvunda Na Umma ukagawika, maovu ukajitenda Sasa wana jakajaka, ili siku ya ulifi Mahuluki bila shaka, huvuna ‘lichopanda Na maji ukiyateka, uyanywe yote mafunda Na koo ikikabika, shauriyo ‘liyaenda Ela watawajibika, ili siku ya ulifi Wacheni kutikatika, kotekote mukiranda Mwakutaka kusifika, wafuasi mwawawinda Mwashinda kunung’unika, na mambo munayapinda Ishara ya kutishika, ili siku ya Ulifi Kama ni kutakasika, ni heri mkatuenenda Ghofira mkatutaka, tukawapa tukipenda Mumwombe Mahuluka, faraja akawatenda Badala ya kutimuka, ili siku ya ulifi Hitaaihirishika, siku ya ndege kupanda Mkayajibu mashtaka, ya zenu ila...