Skip to main content

Siku ya Ulifi


Toka Hegi yasikika, imelia parapanda
Wafike walotajika, wasilimatie kwenda
Majina waliandika, na ila walizotenda
Waache kuhemeka, ili siku ya ulifi

Nawaasa wahusika, waziache propaganda
Hifai kulalamika, kila wanakokuenda
Wengine tope kupaka, jukwaani wakipanda
Wakuache kupayuka, ili siku ya ulifi

Wenyewe waliyataka, mbegu mbaya walipanda
Na chuki waliipika, ikaiva na kuvunda
Na Umma ukagawika, maovu ukajitenda
Sasa wana jakajaka, ili siku ya ulifi

Mahuluki bila shaka, huvuna ‘lichopanda
Na maji ukiyateka, uyanywe yote mafunda
Na koo ikikabika, shauriyo ‘liyaenda
Ela watawajibika, ili siku ya ulifi

Wacheni kutikatika, kotekote mukiranda
Mwakutaka kusifika, wafuasi mwawawinda
Mwashinda kunung’unika, na mambo munayapinda
Ishara ya kutishika, ili siku ya Ulifi

Kama ni kutakasika, ni heri mkatuenenda
Ghofira mkatutaka, tukawapa tukipenda
Mumwombe Mahuluka, faraja akawatenda
Badala ya kutimuka, ili siku ya ulifi

Hitaaihirishika, siku ya ndege kupanda
Mkayajibu mashtaka, ya zenu ila na inda
Nyoyo na zikaponyeka, na makovu yalovunda
Haki itapofanyika, ili siku ya ulifi

Kevin wamalwa
Mlokole Mlumbi
Chuo Kikuu cha Bluefield state,
Marekani



Comments

Popular posts from this blog

Ningekwambia!

Kama ingekuwa vile, swahiba ningeshasema Ningepiga na kelele, ufahamu himahima Kwamba sikuwazi miye, sikomi laili nzima Ningejasiri n’kwambie, lau sikupendi mbuya Kama sivyo ‘ngekwambiya, wazi wazi pasi siri Lau sijasuhubiya, nahari sikufikiri Kwamba sijakuwaziya, na gonezi kuabiri Ngaungama wangu mwari, kwamba siwe nimpendaye Kama kuli mwengineye, ninaye muenendea Mtimangu anitwaliye, ni radhi kumwenendea Hadhi yangu nimpaye, na siwe wangu maridia Ngakwambia siweye, hala ningekuhubiri Kama siwe ulinitwaa, kawa wa kunipa tuo Najenenda nili fwaa, nimetekwa na pumbao Azizi u’vyonivaa, yakaniisha matao Kweli ningeshakujuza, kwamba siwe nyonda

mtu hafi kupenda

Mja hafi kupenda Hapana mja duniani, apenda aondowe Si khiari asilani, rohoye aitowe Aingiye pa gizani, kusiko na mwendowe Maja hafi kupenda, n’ kudura itimiye Ni kudura ya Manani, alompa utuwe Hana na lake Fulani, sema akohowe Hanalo la lakini, zake ziandikiwe Mja hafi kupenda, n’kudura itimiye          Nyaka zikiwa shirini,ni jaala apawe Au aishi theneni, neema ajaliwe Mja hana kwa nini,ikiwa aitiwe Mja hafi kupenda,n’ kudura itimiye Lau ngapewa idhini, k’teuwa atakaye Ngebaki duniani, amwali ajiliye   Afurahi maishani, na wale wampendaye Mja hafi kupenda , n’kudura itimiye

penzi

penzi la kulazimisha,lina gharama, kando na kukalifisha, linakukama, na linakufilisisha, likakukwama, hadi likakubakisha, u litima aimi nakujulisha, uwe salama usipende kujishasha, na kwa lazima penda anorejesha, nayo kheshima huba ja hili hukosha, wako mtima ... mbwene hoa walopenda, kwa kusukuma, hatimaye zao zanda, wakaziuma, kumbe hao walopenda, wamewahama amwalio zimeenda, sa' wamezama