‘Meandika nikujibu, ulouliza mwenzangu
Kwelezeto nastahabu, welewe kauli yangu
Kupenda nini sababu, umenisaili tangu
Sikupendi kwa kupenda, ni kwa kuwa nakupenda
Na maadamu hu bubu, utashiba jibu langu
Kukupenda si ajabu, wan’saliti moyo wangu
Mapenzi yaliusibu, kaubwaga wangu wangu
Sikupendi kwa kupenda, ni kwa kuwa nakupenda
Wala sinistaajabu, hikuwa kupenda kwangu
Ngejua huba lan’karibu, ngelikaa ange kwa rungu
Likija nilidhurubu, lisitwae mtima wangu
Sikupendi kwa kupenda, ni kwa kuwa nakupenda
Navyokupenda habubu, hujapendwa vile tangu
Kwangu uli kama shabu, kunitakasa uchungu
Kan’ridhie nawe hebu, ukubalie hayangu
Sikupendi kwa kupenda, ni kwa kuwa nakupenda
Hukuwazia ghalibu, fikra tele kwa mafungu
Kitamani un’karibu, niwe wako uwe wangu
Viate vyako ‘sababu, vilok’zinga ja magugu
Sikupendi kwa kupenda, ni kwa kuwa nakupenda
Hujui ngapi hesabu, n’mejipinda pali mvungu
N’kililia lako jibu, litalon’toa kiwingu
Uwele likanitibu, mato yaone uwengu
Sikupendi kwa kupenda, ni kwa kuwa nakupenda
Haya ukayaratibu, nilosema kwa vifungu
Uhitimu na kutubu, ukutoke na ukungu
Huu ulokurakibu, unione mwenzangu
Kwani s’pendi tu kupenda, ila kweli nakupenda
Comments